Habari za hivi Punde

KUKOSEKANA KWA MASHINE ZA CD4 ZAWATESA WENYE MAAMBUKIZI YA VVU.

VITUO vya kutolea huduma kwa watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi mkoani Shinyanga vinakabiliwa na changamoto ya upungufu wa mashine za  kupimia CD4 hali inayosababisha hofu kwa watumiaji wa dawa za kufubaza makali   (ARV).


Hayo yalisemwa jana na watoa huduma ya elimu ya VVU na UKIMWI ngazi ya jamii wakati wa warsha ya siku 3  iliyofanyika mjini Kahama   iliyoandaliwa na Shirika lisilo la kiserikali la Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative (AGPAHI) linalojihusisha na mapambano dhidi ya VVU na ukimwi.


Watoa huduma hao walisema mashine za kupimia CD4 katika Vituo vingi vya kutolea huduma  vimekuwa vikiharibika mara kwa mara hali inayosababisha watumiaji washindwe kuelewa maendeleo ya afya zao kwa kuchelewa kupata huduma.


Mmoja wa washiriki wa warsha hiyo Vedastus Mtange kutoka manispaa ya Shinyanga alisema kutokana na kukosekana kwa mashine hizo wanashindwa kubaini kuwa CD4 za mgonjwa zimepanda au zimeshuka hivyo kuiomba serikali kutatua changamoto hiyo haraka ili kuokoa maisha ya watanzania.


“Kuna changamoto ya mashine za kupimia CD4 katika vituo vingi  vya kutolea huduma kwa watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi ,wanapokosa huduma ya vipimo wengine wanaamua kuacha kutumia dawa na kutohudhuria kliniki matokeo yake afya zao zinadhoofika”,alieleza Mtange.


“ Changamoto nyingine ni watumiaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU kutokuwa na anuani sahihi kwani wengine wamekuwa wakiandikisha majina tofauti na yale wanayotumia kwenye maeneo wanayaoshi,hali inayosababisha ugumu katika kufuatilia maendeleo ya afya zao”,aliongeza Mtange.


Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI,Secilia Yona alisema lengo la warsha hiyo ni kuwajengea uwezo watoa huduma ya elimu ya VVU na UKIMWI ngazi ya jamii   ili waweze kuwaunganisha wateja kutoka kwenye ngazi ya jamii kwenda kwenye vituo vya afya.


Akizungumza na mwandishi wa habari  Mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga Dkt Ntuli Kapologwe alisema kuharibika kwa mashine hizo kunatokana  utunzaji kutokuwa mzuri katika vituo sambamba na baadhi ya watoa huduma katika vituo kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu matumizi ya mashine hizo.



 Dkt Kapologwe alisema  pia wanaendelea kutoa elimu kupitia kwa viongozi wa dini,waganga wa tiba za asili na jamii kwa ujumla kuhusu umuhimu wa wateja walioanza kutumia dawa kuhudhuria kliniki mara kwa mara ili kujua maendeleo ya afya zao.


Hata hivyo alisema bado kuna changamoto kwa baadhi ya wananchi kuamini katika imani za kishirikina kwamba hajaambukizwa VVU hivyo wanaacha tiba waliyoanza na kukimbilia kwa waganga wa jadi kitendo ambacho alisema kinasababisha baadhi ya wateja kupotea katika huduma.


0 Response to "KUKOSEKANA KWA MASHINE ZA CD4 ZAWATESA WENYE MAAMBUKIZI YA VVU."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.