Habari za hivi Punde

WAZAZI NA WALEZI WALAUMIWA KUWATELEKEZA WATOTO WAO KATIKA KITUO CHA KULELEA WATOTO WALEMAVU





WAZAZI  na walezi  waliopeleka watoto wao katika kituo   maalumu cha  kulelea  watoto wenye ulemavu  mbalimbali kilichopo  Buhangija manispaa ya Shinyanga wameombwa kujenga desturi ya kuwatembelea watoto  hao mara kwa mara na sio kukiachia  kituo pekee hali ambayo inawafanya  kukosa haki zao za msingi  kwa kupata malezi bora kama watoto wengine.

Baadhi ya watoto hao tangu waletwe kituoni hapo  hakuna hata mzazi au mlezi mmoja aliyekuja katika kituo hicho kumuona mwanaye  na kumjulia hali  jambo ambalo linaonywesha kuwa watoto tayari wamekosa imani na wazazi wao kwa kutowaona muda mrefu.


Hali hiyo ilijionyesha wakati  familia ya Mwalongo  ilipokwenda   kutoa msaada wa  vyakula mbalimbali kwaajili ya  kusherekea sikukuu ya pasaka   ikiwemo mbuzi wanne,kilo mia moja za mchele na lita 20 za mafuta ya kupikia  vyenye  thamani ya  zaidi ya shilingi laki tatu  na kuvigawa katika kambi za kituo cha Buhangija na kituo cha Kolandoto cha  kulelea wazee wenye ukoma    ikiwa ilibainika kuwa   idadi kubwa ya watoto wenye ulemavu wa ngozi kutokwenda makwao  kutokana  na hofu ya kuuwawa.

Mlezi wa  kituo hicho Maisala Adinani alisema kuwa  hali iliyopo kweli baadhi ya wazazi au walezi wamekuwa wakishindwa kuja kuwaona watoto wao kuna wengine tangu waletwe  imefika miaka saba hawajawahi kuwaona wazazi wao ama kuwatembelea na kuwajulia hali.

Ikiwa  imeelezwa kuwa   idadi ya watoto walipo ni 258 kati ya hao wenye ulemavu wa ngozi (Albino) ni 172,wasioona 48 na viziwi ni 38  ambapo kila  baada ya wiki moja mtoto analetwa ndani ya kituo hicho na wazazi kutofika ili  kuwajulia hali hata kipindi hiki cha siku kuu ya pasaka.
 
Naye katibu wa chama cha  wasioona manispaa ya Shinyanga  Richard  Mpongo alisema kuwa  tabia ya wazazi  kuwatelekeza watoto katika kituo hicho sio jambo la hekima huko ni kuwanyima haki zao za msingi kama wazazi na kufanya watoto hao kukosa upendo,hivyo jamii imetakiwa kuondoa dhana ya mauaji  na kuwatenga walemavu  huku wakiwafanya kusihi maisha ya mashaka na hofu kubwa.

Mmoja wa wanafamilia hiyo Anna Mwalongo alisema kuwa wameguswa na kundi hilo lisilojiweza kwani jamii imekuwa ikiwatenga  na kuwauwa  hivyo serikali inatakiwa kukemea kwa nguvu zote ,pia wazazi wao  wasiwatelekeze  wawaone kuwa na umuhimu kama watoto wengine  ikiwa  wamekuwa wakikosa mambo ya msingi kwa wazazi ikiwemo upendo.

Aidha  mmoja wa  watoto  wanaolelewa katika kituo hicho wenye ulemavu wa ngozi  Hassani   Khamis  alisema kuwa  yeye ni mmoja wa kutelekezwa na wazazi  alizaliwa wilayani Kahama lakini tangu aletwe na wazazi katika kituo hicho imekuwa ni shida kuwaona  hata akiwa  mgonjwa   hawatokei kumujulia hali yake.

0 Response to "WAZAZI NA WALEZI WALAUMIWA KUWATELEKEZA WATOTO WAO KATIKA KITUO CHA KULELEA WATOTO WALEMAVU"

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.