Habari za hivi Punde

kIJANA ACHOMWA KISU NA KUFA KISA ATAKA KUMBAKA MSICHANA.



KIJANA  mmoja (30) aliyejulikana kwa jina la Stephen Philbert ameuawa kwa kuchomwa kisu kichwani na mwanamke  aliyekuwa anamfanyia jaribio la kumbaka  katika eneo la Ngokolo mjini Shinyanga usiku wa mkesha wa pasaka.

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga SACP Evarist Mangalla alisema tukio hilo limetokea usiku wa Aprili 20,mwaka huu saa tisa usiku ambapo Stephen Philbert mkazi wa Ngokolo alichomwa kisu kichwani wakati akitaka kumbaka mwanamke aitwaye Pili Michael(24).

Akielezea zaidi kuhusu tukio hilo kamanda Mangalla alisema siku ya tukio mwanamme huyo alivunja dirisha la nyumba ya mwanamke huyo anayeishi Ngokolo mjini Shinyanga na kuingia ndani kisha kufanya jaribio la kumbaka.


“Kwa mujibu wa maelezo ya Pili Michael,ni kwamba baada ya dirisha lake kuvunjwa na marehemu aliingia ndani na kufanya jaribio la kumbaka ndipo katika kujihami kwake alimchoma kisu kichwani”,alieleza kamanda Mangalla.

Kamanda Mangalla aliongeza kuwa mwanamme huyo baada ya kuchomwa kisu kichwani alipiga kelele watu wakaja kumsaidia na kumpeleka hospitali ya mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya matibabu lakini akafariki dunia akiwa katika hospitali hiyo.

Alisema tayari jeshi la polisi linamshikilia mwanamke aliyefanya mauaji hayo kwa mahojiano zaidi kuhusu tukio hilo.

Hata hivyo kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya mkoa wa Shinyanga Dkt Maguja Daniel alisema hospitali hiyo haina taarifa kuhusu mwanamme huyo aliyeuawa kufikishwa hospitalini hapo.


0 Response to "kIJANA ACHOMWA KISU NA KUFA KISA ATAKA KUMBAKA MSICHANA."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.