Habari za hivi Punde

DIWANI WA CCM KATA YA LUPINGU- LUDEWA MKOANI IRINGA AFARIKI KWA AJALI.

Gari aina ya Toyota Coaster iliyokuwa ikifanya safari zake kutoka Ludewa Mjini kuelekea Lupingu baada ya kupata ajali iliyoondoa uhai wa Diwani wa Viti Maalum CCM Kata ya Lupingu, Prisca Kayombo (Zaruta).
Diwani wa Viti Maalum CCM Kata ya Lupingu, Prisca Kayombo (Zaruta) wa  tatu  kushoto enzi za uhai wake  akiwa na Mbunge wa Jimbo la Ludewa, Deo Filikunjombe (wa kwanza kushoto), Katibu wake Stan Gowele (wa pili kushoto) na wananchi  wengine wa Ludewa wakijiandaa kunyanyua nguzo ya umeme wiki mbili zilizopita.
Baadhi ya majeruhi wa ajali hiyo wakiwashushwa katika Hospitali ya Wilaya Ludewa, mkoani Iringa leo.
Majeruhi wakiwa katika Hospitali ya Wilaya Ludewa.
Wananchi wa Kata ya Ludewa wakiwa hospitalini hapo kuwaona majeruhi wa ajali.
DIWANI wa Viti Maalum CCM Kata ya Lupingu, Prisca Kayombo (Zaruta) amekufa papo hapo huku watu wengine kadhaa wakijeruhiwa vibaya katika ajali mbaya ya gari iliyotokea leo asubuhi huko Ludewa mkoani Iringa.
Mashuhuda wa ajali hiyo walidai kuwa chanzo chake ni gari hilo ambalo walikuwa wakisafiria kutoka Lupingu - Ludewa kufeli breki na hivyo kupinduka .
Inadaiwa baada ya gari hilo aina ya Toyota Coaster inayojulikana kwa jina la DMX kufeli breki dereva aliwataka abiria kutulia ndani ya gari hilo ila diwani huyo hakuweza kufanya hivyo na kuamua kuchukua maamuzi magumu ya kutaka kuruka katika gari hilo ambapo wakati akiruka alimsukuma utingo wa basi hilo na hivyo wote wawili utingo na diwani kufunikwa na gari hilo na kupelekea kifo cha diwani huku utingo akiwa mahututi baada ya kubanwa na gari hilo.
"Diwani amepoteza maisha wakati akiwa njiani kuelekea kujumuika na wananchi wake katika shughuli ya maendeleo ya kuchimba mashimo ya nguzo za umeme kuelekea kijijini kwake Lupingu" Alisema mmoja wa abiria.
Mbunge wa Jimbo la Ludewa, Deo Filikunjombe ameeleza kusikitishwa na kifo cha diwani huyo kutokana na mchango wake mkubwa aliouonyesha enzi wa uhai wakati kwa kushiriki vema na wananchi wa kata yake katika zoezi la kufyeka na kuchimba mashimo ya nguzo za umeme kwenda Lupingu.
Alisema kuwa anakumbuka ni wiki mbili pekee zimepita toka diwani huyo alipoungana nae katika uchimbaji wa mashimo ya nguzo za umeme kwenda kijiji cha Ntumbati na kuwa hata wakati ajali hiyo inamkuta bado alikuwa katika harakati za kuwatumikia wananchi wake.
"Ludewa tumempoteza diwani mchapa kazi na aliyependa kujituma muda wote na hata wakati mwingine diwani huyo alikuwa akifanya kazi ngumu kama mwanaume kwa kubeba nguzo za umeme kwa kushirikiana na mimi na wananchi wake.....kwa kweli kifo chake ni pigo kubwa ndani ya CCM na kwa wananchi wa kata nzima ya Lupingu"
Kwani kati ya madiwani waliokuwa bega kwa bega na wananchi wao na mbunge ni pamoja na diwani huyo ambaye alikuwa mstari wa mbele kuona Kata ya Lupingu inapata umeme wa uhakika baada ya miaka zaidi ya 50 ya Uhuru bila umeme .
Mbunge Filikunjombe alisema atamkumbuka diwani huyo kutokana na mchango wake mkubwa katika maendeleo na vile alivyofanya kazi na wananchi wote bila kujali itikadi zao za vyama.

Mkuu wa wilaya ya Ludewa, Juma Madaha amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo iliyosababisha kifo cha diwani huyo na kuwa ajali hiyo ilitokea majira ya saa 2 asubuhi .
(PICHA / STORI: FRANCIS GODWIN, IRINGA)

0 Response to "DIWANI WA CCM KATA YA LUPINGU- LUDEWA MKOANI IRINGA AFARIKI KWA AJALI."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.