Habari za hivi Punde

MBOWE LEO AUNGURUMA MJINI DODOMA CHINI YA ULINZI MKALI WA POLISI.


Dar/Dodoma. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe leo atasindikizwa na mawakili watano atakaporipoti Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, Dar es Salaam alikoitwa kuhojiwa kuhusu kauli yake ya kuitisha maandamano nchi nzima kushinikiza kusitishwa kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Mawakili hao wataongozwa na Makamu Mwenyekiti wake, Profesa Abdallah Safari, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, Halima Mdee, Mabere Marando na Peter Kibatala, huku makada wa chama hicho wakialikwa kuandamana naye kumsindikiza.
Mbowe alitoa kauli hiyo katika Mkutano Mkuu wa chama hicho Septemba 14, mwaka huu, akisema maandamano hayo yatafanyika katika siku ambayo itapangwa katika mikoa yote.
Siku moja baadaye, Mkuu wa Operesheni na Mafunzo wa Polisi, Kamishna Paulo Chagonja alimkemea akisema iwapo atafanya hivyo, hatua za kisheria zitachukuliwa. Pia, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) alimwandikia barua akimwita kuhojiwa.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema jana kwamba uamuzi huo ni moja ya maazimio matatu ya kikao cha kwanza cha Kamati Kuu (CC) ya chama hicho iliyokutana Dar es Salaam juzi.
“Mbowe ameitwa Makao Makuu ya Jeshi la Polisi kesho (leo). Polisi wameandika barua ya wito huo lakini hawajasema kosa lake ni nini. Itakuwa saa tano asubuhi na atakwenda na mawakili wote wa chama,” alisema Dk Slaa mbele ya viongozi wote wa sekretarieti mpya ya chama hicho.
Akizungumzia wito huo jana, DCI Mngulu alisema ingawa leo atakuwa Songea, ofisi yake ina watumishi wengi na kwamba ameshawasiliana naye kwa ujumbe kumfahamisha hilo.


Katika mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Bara), John Mnyika alisema, “Tunawaomba wanachama wa Chadema kujitokeza Makao Makuu ya Polisi ili kumsindikiza mwenyekiti atakayekuwa akihojiwa.”
Kwa upande wake, Lissu alisema katika barua ya wito, polisi wametaja vifungu vya sheria, lakini hawakueleza kosa la Mbowe ni nini, jambo ambalo linaonyesha jinsi wanavyofanya kazi nyuma ya kivuli cha chama tawala, CCM.
Akizungumzia madai hayo, Mngulu alisema Kifungu cha 10 cha Sheria ya Makosa ya Jinai kinajieleza wazi. Kifungu hicho kinazungumzia kudhamiria kutenda kosa.
Maandamano
Akizungumzia maandamano hayo, Dk Slaa alisema tarehe rasmi itatajwa baada ya viongozi wa Ukawa kukutana... “Maandamano yatafanyika nchi nzima, tayari taratibu zimeanza kufanywa mikoani. Tutaeleza tarehe hiyo. Tumepinga kwa maneno tukitaka Bunge lisitishwe lakini wenzetu wameweka pamba masikioni. Sasa tunaonyesha chuki na hasira, polisi watambue kuwa wao wapo 35,000 na wananchi wapo milioni 45.
“Tumenyimwa vibali katika mikutano yetu iliyopita sasa safari hii wakikataa kutupa kibali tutaandamana tu. Azimio la Kamati Kuu haliwezi kuvunjwa na Chagonja kwa sababu maandamano ni haki yetu na tumeshafanya maandamano 100 ya amani nchini.”
Ukawa
Kuhusu ushirikiano wa vyama vinavyounda Ukawa, Dk Slaa alisema hilo ni azimio la pili la Kamati Kuu ambayo imebariki ushirikiano huo kuanzia katika Uchaguzi wa Serikali za Mtaa na Uchaguzi Mkuu 2015.
“Kamati Kuu imeunda kamati ndogo itakayoongozwa na Profesa Safari ikiwajumuisha Benson Kigaira, Mnyika na John Mrema kuangalia namna ushirikiano huo utakavyokuwa. Kamati hiyo imeanza kazi leo (jana),” alisema.
Alisema azimio la tatu la Kamati Kuu ni kuhakikisha kuwa Ukawa wanaidai Katiba ya wananchi na kwamba wanatembea nchi nzima kueleza uchakachuaji wa Rasimu ya Katiba uliofanywa na CCM bungeni.
LHRC yawavaa polisi
Katika hatua nyingine, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimesema Jeshi la Polisi limekurupuka kuzuia wafuasi wa Chadema kuandamana kupinga kuendelea kwa vikao vya Bunge wakati chama hicho hakijatoa taarifa rasmi kwa jeshi hilo.
Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Uwajibikaji wa kituo hicho, Imelda Urio alisema alichofanya Mbowe ni kutangaza kusudio la kufanya maandamano na kwamba hatua nyingine za kutoa taarifa rasmi kwa jeshi hilo zingefuata baadaye.

0 Response to "MBOWE LEO AUNGURUMA MJINI DODOMA CHINI YA ULINZI MKALI WA POLISI."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.