Habari za hivi Punde

WANAFUNZI WASIOONA (WENYE UPOFU) WATUMIA VIFAA VIBOVU KUJIFUNDISHIA KUANDIKA NA KUSOMA KITUO CHA BUHANGIJA SHINYANGA

Ndani ya moja ya madarasa lenye wanafunzi wasioona-Pichani ni mwalimu Agnes Makambajeki akiwa na wanafunzi wake wakijifunza kwa kutumia vifaa ambavyo vinaelezwa kuwa ni vibovu.

 

Wanafunzi wasioona wanaosoma katika shule ya msingi Buhangija Jumuishi katika manispaa ya Shinyanga wanakabiliwa na upungufu wa mashine za kujifunzia hali ambayo inaelezwa kuwapa wakati mgumu walimu wanaowafundisha.

Hayo yamebainishwa jana na mkuu wa kitengo cha watoto wenye ulemavu katika kituo hicho Bright Mduma ambapo alisema hivi sasa watoto wasioona wapo 38,  wavulana 25 na wasichana 13,lakini mashine za kujifunzia zinazotumika ni 8 pekee kati ya 28 zilizopo.

Mduma alieleza kuwa kati ya mashine 25 za wasioona nzima ni 8 pekee,20 ni mbovu na wamekuwa wakizitengeza mara kwa mara hivyo kuwaomba wadau wa elimu na watoto kujitokeza kusaidia watoto hao.

“Tuna upungufu wa vifaa kwa watoto wasioona,mashine za wasioona( Perking Brailler) nyingi zimeharibika,hata karatasi na kalamu maalum kwa wasioona hazitoshi”,aliongeza Mduma.

Katika hatua nyingine mkuu huyo wa kitengo alitaja changamoto nyingine kuwa ni upungufu wa meza na viti kwa wanafunzi na walimu wanaofundisha watoto hao.

Kwa upande wake mwalimu  anayefundisha watoto hao Agnes Makambajeki aliiomba serikali na wadau wengine kufika katika kituo hicho ili waone mazingira yasiyo rafiki kwa wanafunzi hao ili waone umuhimu wa kuwasaidia.

Naye mwalimu mkuu msaidizi katika shule hiyo Pius Lukala alisema walimu wanaofundisha watoto wasioona ni watatu pekee na wanahitajika walimu wawili ili wawe watano wafundishe kuanzia darasa la kwanza hadi la saba.

Shule ya msingi Buhangija  Jumuishi iliyopo katika kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa ngozi,wasioona na wasiosikia hivi sasa ina watoto 275, wasioona 38,wasiosikia 49 na wenye ulemavu wa ngozi 188.

Pamoja na shule hiyo kuwa na wanafunzi wenye ulemavu pia wapo wanafunzi wasiokuwa na ulemavu 758.
Na Marunde  Kadama.

 
 


0 Response to "WANAFUNZI WASIOONA (WENYE UPOFU) WATUMIA VIFAA VIBOVU KUJIFUNDISHIA KUANDIKA NA KUSOMA KITUO CHA BUHANGIJA SHINYANGA"

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.