Habari za hivi Punde

MWILI WA BINADAMU ULIOKAA MOCHWARI KWA ZAIDI YA SIKU 50 HATIMAYE UMEZIKWA KIMYAKIMYA -MKOA WA KILIMANJARO MOSHI


Hatimaye mwili wa Rosemary Marandu uliohifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Rufaa ya KCMC kwa siku 53 umezikwa huku maziko hayo yakigubikwa na utata na kuhudhuriwa na wanaume sita.
 
Mazishi hayo yalifanyika juzi saa 10:30 jioni katika Makaburi ya Karanga mjini hapa na hakuna aliyehudhuria kati ya baba wala mama wa marehemu.

Taarifa za kufanyika kwa siri kwa maziko hayo zililifikia gazeti hili saa 10:40 jioni na waandishi walipofika makaburini, waliambulia kukuta mishumaa iliyokuwa ikiwaka ikiwa imewekwa juu ya kaburi na hakukuwa na mtu hata mmoja.

Mashuhuda wa tukio hilo, waliozungumza na gazeti hili, walidai kuwa waliyaona magari mawili yakiingia makaburini hapo, moja likiwa limebeba maiti na kushuhudia watu sita wakishuka katika magari hayo ambao waliuzika mwili huo.

Hata hivyo, bado kuna utata kuhusu nani hasa aliyefanya maziko hayo baada ya baba wa marehemu kudai ni mtoto wa marehemu aitwaye Witness Marandu na mkewe Felicia akikanusha.

Maziko hayo yamefanyika ‘chapchap’ wakati marafiki wa karibu na Marandu walipokuwa katika jitihada za mwisho za kumshawishi aukabidhi kwa mama wa marehemu juzi mchana ili auzike.


Kauli ya Baba wa Marehemu

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu juzi usiku kutoka wilayani Rombo, baba wa Rosemary, Flavian Marandu alisema mtoto wa marehemu aliyemtaja kwa jina la Witness Marandu (17), ndiye aliyeuchukua mwili huo na kwenda kuuzika.

Marandu alisema mtoto huyo alimfuata akiwa amefuatana na ndugu wengine ambao hakuwataja akiomba apewe mwili wa mama yake ili akauzike.

Alidai kuwa awali aliwapa uhuru wa kuchagua sehemu ya kwenda kuzika katika moja ya mashamba yake yaliyoko Kitirima Kingachi wilayani Rombo au katika makaburi ya umma watakayoona yanafaa.
Marandu alisema baadaye akiwa amepumzika akiugulia maumivu ya kutoa jino, wanaukoo hao pamoja na mtoto wa marehemu walimpigia simu na kumshukuru kwamba wameshazika salama.

Mgogoro huo wa kugombea maiti ni wa pili kuhusisha ukoo wa akina Marandu, miaka takriban 10 iliyopita, maiti nyingine ya mwanaukoo huo ilikaa mochwari kwa zaidi ya siku 90 baada ya kutokea mgogoro unaofanana na huo.
Mama ageuka mbogo
Hata hivyo Felicia Nkya ambaye ni mama mzazi wa marehemu aliliambia gazeti hili si kweli kuwa mjukuu wake (Witness) ndiye aliyeuchukua mwili huo na kwenda kuuzika.
Alisema madai ya mumewe kuwa mjukuu huyo alimfuata juzi kuomba akauzike mwili huo hayana ukweli kwani mpaka siku hiyo, Witness alikuwa yuko shuleni mkoani Mbeya.

0 Response to "MWILI WA BINADAMU ULIOKAA MOCHWARI KWA ZAIDI YA SIKU 50 HATIMAYE UMEZIKWA KIMYAKIMYA -MKOA WA KILIMANJARO MOSHI"

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.