Habari za hivi Punde

TAMICO YATARAJIA KUWABURUZA MAHAKAMANI VIONGOZI WAANDAMIZI BULYANHULU.



 Na  Kareny   Masasy
Shinyanga.

CHAMA  cha wafanyakazi wa migodi, nishati, ujenzi na kazi nyinginezo (TAMICO) kinatarajia kuwafikisha mahakamani viongozi waandamizi wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu unaomilikiwa na African Barrick Gold mine,(ABG) kwa tuhuma za kuwashawishi watumishi wa mgodi huo kusitisha uanachama wa chama hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake, mjini Shinyanga, katibu wa TAMICO, kanda ya magharibi, Benjamini Dotto alisema walifikia uamuzi huo kufuatia uongozi wa Mgodi kusambaza fomu maalumu kwa watumishi hao ikielekeza kuwashawishi kujiondoa uanachama TAMICO.

Aliwataja viongozi hao kuwa ni pamoja na meneja mkuu wa mgodi huo, Peter Burger, meneja kitengo cha mahusiano kazini rasilimali watu, Onesmo Kabeho, meneja kitengo cha rasilimali watu, Antony Mosha na  meneja ustawi wa kampuni hiyo, Gath Boersma.

Alisema kwa pamoja viongozi hao wametumia nafasi zao za uongozi kuwashawishi wafanyakazi wapatao 651, kusitisha uanachama wao TAMICO kwa maslahi yao binafsi ikiwemo kuaandaa namna ya kuwafukuza kazi na kuwanyima haki zao.

“Tumeamua kuwafikisha mahamani kutokana na na viongozi hao kuwashawishi wafanyakazi kusitisha uanachama TAMICO ambapo januari 10, mwaka huu Bw. Mosha aliwasainisha barua hizo watumishi 375 kwa barua yenye kumbukumbu namba, BGML/HR/2014” alisema katibu huyo.

Aidha, alimtaja mwingine kuwa ni meneja ustawi wa kampuni hiyo, Gath Boesma, ambaye aliwasainisha watumishi 214, novemba 9, mwaka jana, kwa barua yenye kumbukumbu namba BGML/HR/2013 na watumishi 62 kwa barua yenye kumbukumbu namba BGML/HR/2013 ya novemba 8 mwaka jana
 Katika hatua nyingine, katibu huyo alisema (TAMICO) imefungua kesi mbili dhidi ya kampuni hiyo ya madini katika tume ya usuluhisi na uamuzi(CMA) mjini Shinyanga.

  Alizitaja kesi hizo kuwa ni pamoja na kesi ya kwanza yenye kumbukumbu namba CMA/SHY/3/2014 kikiwa chama hicho kinaiomba tume ibatilishe notisi ya mwajiri aliyoitoa kwa chama ikiwa na kusudio la kuvunja mkataba wa utambuzi ambapo katika kesi ya pili yenye kumbukumbu namba CMA/SHY/4/2014 chama kinaomba kukamilishwa na kufungwa kwa mkataba wa hali bora iliyotakiwa kufanya hivyo tangu mwaka 1999.

Katibu huyo wa TAMICO kanda ya magharibi alisema chama hicho kilifikia maamuzi hayo baada ya kugundua kwamba uongozi wa kampuni hiyo ya Bulyanhulu haukufuata taratibu za kisheria, katika kufikia hatua ya kutoa notisi ya kuvunja mkataba wa utambuzi ambapo pia mwajiri amechelewesha kumalizika kwa majadiliano ya mkataba wa hali bora hivyo kuwanyima nafasi wafanyakazi ya kuongezeka kwa maslahi yao.

Aidha, Bw. Dotto alifafanua kuwa mwajiri huyo ameonesha nia mbaya katika kuvunja mkataba huo kwa kutengeneza fomu hizo haramu ambazo kwa kushirikiana na kikundi alichokiita haramu cha NUMET wamekuwa wakiwaondolea wafanyakazi nguvu ya kujadiliana.

 

0 Response to " TAMICO YATARAJIA KUWABURUZA MAHAKAMANI VIONGOZI WAANDAMIZI BULYANHULU."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.