VYUMBA 20 vya bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari ya African Muslim, iliyoko Kata ya Kaloleni, Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, vimeteketea kwa moto.
Moto huo ambao ulizuka juzi saa 1:45
jioni na kuwaka kwa zaidi ya saa tano, ulianzia katika choo cha shule
hiyo, jirani na Bweni la Makka kabla ya kuruka kwenye chumba cha jirani
na kusambaa kwenye vyumba 20 vilivyoko katika bweni hilo.
Akizungumza toka eneo la tukio,
Mkurugenzi wa Shule hiyo, Ali Adam Ali, alisema moto huo ambao hadi sasa
chanzo chake hakijajulikana japo inadaiwa kuwa ni hitilafu ya umeme,
umesababisha hasara kubwa kwa wanafunzi zaidi ya 96 wa kidato cha nne
wanaotumia bweni hilo.
“Moto huu ulianza majira ya saa
mbili kasoro, wanafunzi walikuwa wanajiandaa kuingia katika swala ya
Isha, mmoja wa wanafunzi alihisi harufu ya moto na kuwajuza wenzie,
baadae wakaanza kuhangaika kutafuta ni wapi chanzo chake kilipo,
waligundua kuwa ulianzia chooni, ghafla ukasambaa katika vyumba vingine
vya ghorofani kupitia chumba cha jirani na choo,” alisema Ali.
Alisema hakukuwa na madhara makubwa
yaliyotokana na moto huo kutokana na wanafunzi wengi kuwa likizo, na
kwamba ni wanafunzi wa kidato cha nne na kidato cha pili tu ndio
walioathirika na moto huo.
“Hakuna majeraha makubwa kutokana
na tahadhari ya kiusalama tuliyochukua kwa kushirikiana na uongozi wa
Serikali ya Mtaa, wanafunzi walijitahidi kuondoa vitu vyao, vitanda na
mabegi ya baadhi yao vimeungua katika moto, wanafunzi wanne walipoteza
fahamu, tuliwakimbiza hospitali na sasa wanaendelea vizuri,”alisema Ali.
Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na
Usalama wa Mkoa, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Dkt. Ibrahim Msengi,
aliuagiza uongozi wa shule hiyo kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa
Manispaa na Ofisa Elimu wa mkoa kufanya tathimini ya hasara iliyotokana
na moto huo.
Wakati huo huo, Kaimu Ofisa Elimu
Mkoa wa Kilimanjaro, Estomih Makyara amemtaka mkurugenzi wa shule hiyo
kutoa wiki moja ya mapumziko kwa wanafunzi walioathirika na moto huo,
isipokuwa wanafunzi wa darasa la saba wanaoendelea na mitihani
wataendelea kama kawaida.
0 Response to "MOTO WATEKETEZA BWENI LA WASICHANA SEKONDARI YA AFRICAN MUSLIM -KALOLENI MOSHI"
Post a Comment