Habari za hivi Punde

WATU WANNE WA FAMILIA 1 WAKAMATWA WAKILIMA UCHI SHAMBANI

Jeshi la polisi  Mkoani Simiyu linawashikilia watu wanne wa familia
moja kwa tuhuma ya kukutwa wakilima uchi wa mnyama shambani kwa kile
kinachodaiwa  kuwa ni imani za kishirikina.

Kaimu kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Simiyu Venansi Kimario
alisema tukio hilo limetokea septemba 2 majira ya saa 12 asubuhi
katika kijiji cha Bushikwamala kata ya Kalemela wilayani Busega Mkoani
Simiyu

Kimario alisema kuwa watu hao walikamatwa na jeshi la polisi alfajiri
huko Bushigwamhala wakiwa wanalima kwenye shamba lao na walipohojiwa
walidai kuwa walielekezwa na babu yao kipindi cha uhai wake kuwa
wakilima uchi watapata mavuno  mengi.

Kamanda Kimario aliwataja waliokamatwa kuwa ni Makoye Kagoje (42), na mke
wake Neema Kigwela (31) pamoja na watoto wao, mmoja wa kiume (15) na
wa kike (12) majina yamehifadhiwa.

Aidha Kimario alisema watu hao pamoja na watoto wao wanashikiliwa na
jeshi la polisi kwa kukutwa wakifanya vitendo vya ushirikina.

Babu yao alishafariki mwaka jana na aliwaambia kuwa wakilima wapo uchi
watapata mavuno mengi, hivyo waliamua kufanya hivyo kutokana na wosia
wa babu yao

Alisema baada ya jeshi la polisi kupata taarifa kutoka kwa raia wema
liliweza kufika katika eneo hilo na kuwakamata watuhumiwa hao wakiwa
wanaendelea kulima bila nguo.

Hata hivyo Kimario amewataka watu wasijishirikishe kwenye
vitendo vya ushirikina na siyo kwamba ukilima uchi utapata mazao mengi
tofauti na kufuata kanuni za kilimo bora, viongozi wa madhehebu ya
dini na viongozi wa serikali tuwaelimishe watu waachane na imani za
kishikina .

Na Faustine Fabian-Simiyu



0 Response to "WATU WANNE WA FAMILIA 1 WAKAMATWA WAKILIMA UCHI SHAMBANI"

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.