Habari za hivi Punde

WATU WATANO WAHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA 37 KWA WIZI WA BENK YA NMB- WILAYANI MASWA

HAPA NI NJE YA MAHAKAMA WATU WA MANISPAA YA SHINYANGA WALIVYOKUWA WAMEFURIKA
MAHAKAMA   ya hakimu mkazi wa Mkoa wa Shinyanga imewahukumu watu  watano kifungo cha miaka 37 na Viboko 24 kila mmoja  baada ya kupatikana na hatia ya kuvamia na kupora Benki ya NMB tawi la Maswa kwa kutumia silaha.

Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo Neema  Gasabile aliwahukumu kifungo cha miaka 37 na Viboko 24 kila mmoja viboko 12 wakati wa kuingia na 12 wakati wa kutoka baada ya kuridhika na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashitaka kuwa kwa pamoja walitenda kosa hilo kinyume cha sheria.

Washitakiwa hao ni Kapama Hamis Ramadhan (37), Mussa Athuman Buberwa (38), Amos Mathayo,  Lucas Vicent Mabela (40)na Zainabu Mchau (60) wote kwa pamoja walipatikana na hatia ya makosa tisa ya jinai.

Mbele ya Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo,  Mwendesha mashitaka Mwanasheria wa Serikali Edith  Tuka aliieleza Mahakama hiyo kuwa washitakiwa wote kwa pamoja walitenda kosa hilo majira ya saa 6:00 mchana Julai 5, mwaka 2010 mjini Maswa.

Akifafanua mashitaka hayo Tuka alisema kuwa mara baada ya kuvamia ndani ya benki hiyo washitakiwa waliwashambulia askari wa Polisi kwa Silaha na kuwajeruhi kwa kipigo baadhi ya wafanyakazi  na wateja wa benki hiyo.

“Mbali na Vitendo vya kuwashambulia na kuwajeruhi Askari wa polisi, Wafanyakazi na baadhi ya wateja wa benki hiyo lakini pia watuhumiwa waliteka gari aina ya Land rover 109 iliyotumika katika uvamizi huo kisha wakapora fedha taslimu na mali nyingine ambayo thamani yake bado haijajulikana”  alisema  Mwendesha mashitakaTuka.
 
Akifafanua kuhusu mashitaka yaliokuwa yanawakabili washitakiwa hao kabla ya kifungo hicho Tuka alisema  ni pamoja na kufanya uporaji  wa kutumia nguvu na silaha, kumiliki silaha bila kibali cha serikali, kujeruhi, kuteka gari na kupora mali na fedha katika siku na muda uliotajwa mjini  Maswa.

Kwa upande wa mashitaka uliwasilisha mashahidi 24 na  vielelezo mbalimbali ikiwamo Vipimo vya Vinasaba (DNA)  Vilivyowahusisha  watuhumiwa  na tukio hilo.

Awali Mwendesha mashitaka huyo aliiomba Mahakama  kutoa adhabu kali kwa washitakiwa ili iwe fundisho kwa watu wengine wanaotenda makosa kama hayo kwa kuwa hivi sasa vitendo hivyo vimeshamiri nchini.

Mamia ya wakazi wa Mkoa wa Shinyanga walifurika ndani na nje ya Mahakama hiyo iliyokuwa chini ya ulinzi mkali wa askari  Polisi na Magereza kushuhudia hukumu yenye kurasa 200 iliyosomwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo aliyoisoma kwa takriban saa tatu.

0 Response to "WATU WATANO WAHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA 37 KWA WIZI WA BENK YA NMB- WILAYANI MASWA"

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.