Habari za hivi Punde

WANANCHI GAIRO WACHOMA MOTO OFISI YA MTENDAJI WA KATA.

 
WANANCHI wa Kata ya Chakwale Wilaya ya Gairo mkoani hapa, wamechoma moto na kuteketea kabisa, Ofisi ya Ofisa Mtendaji wakimtuhumu kuhusika na ubadhirifu wa fedha, kuwanyanyasa na kuwaweka ndani pindi wanapofuatilia michango mbalimbali ya maendeleo.
Baadhi ya wakazi wa Chakwale waliohojiwa kwa nyakati tofauti baada ya tukio hilo, walisema wananchi hao walichukua uamuzi huo kwa jazba, kutokana na manyanyaso ya muda mrefu yaliyokuwa yakifanywa na Mtendaji Hamza Mbalale, ambaye amekuwa akitumia mabavu kuwaongoza kwa mgongo wa kulindwa na baadhi ya viongozi wa juu serikalini katika Wilaya hiyo.
Kwa masharti ya kutotajwa majina yao, wananchi hao walisema Mtendaji huyo alikuwa akidiriki kuwafuata wananchi wakiwa kwenye majukumu yao yakiwemo ya kazi na kuwakamata na kuwaweka ndani, akiwalazimisha kutoa michango ya shule, mambo ambayo wanaamini yangeweza kufanyika kwa mazungumzo na ushawishi.
Akizungumzia tukio hilo kwa njia ya simu, Mtendaji huyo alisema tukio hilo la kuchomwa moto kwa ofisi hiyo lilitokea mwishoni mwa mwezi uliopita majira ya usiku, muda mchache baada ya kuwa amekwenda polisi kutoa taarifa za fujo zilizoanza kujitokeza baada ya kuwekwa ndani kwa watu walioshindwa kuchangia michango ya maendeleo ya kata.
Alisema, kikubwa wananchi wa Kijiji cha Chakwale wamekuwa na usumbufu mkubwa wa kuchangia shughuli mbalimbali za maendeleo, ambako kwa mujibu wa maazimio ya mikutano mikuu ya vijiji, ilimriwa kila mwananchi mwenye miaka 18 hadi 60, alipaswa kuchangia sh 5,000 kwa mradi mmoja wa maendeleo.
Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Hanifa Karamagi, hakuweza kupatikana kuzungumzia tukio hilo baada ya simu yake kuita bila kupokewa.

0 Response to "WANANCHI GAIRO WACHOMA MOTO OFISI YA MTENDAJI WA KATA."

Post a Comment

KARENY. Powered by Blogger.